Siku ya Tatu: Kuwa Dhahiri

Uncategorized January 9, 2025

Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba”

Mathayo 6:7,8

Omba kwa Dhati

Mwanetu, Ovidiu, alinunua nyumba kwa bei ya chini sana, lakini nyumba hiyo ilikuwa duni na ndogo sana. Ilimlazimu kuirekebishe na kuipanua ili kutosheleza mahitaji ya familia yake. Lakini, bei zilipanda sana. Alisema mara kwa mara hata kukawa na uwezekano mkubwa kutoweza kukamilisha kazi hiyo kutokana na ukosefu wa fedha.

Nilimtaka Ovidiu kuwasilisha mahitaji yao mbele za Mungu kwa sababu Anawajali. Alijibu kwamba ameomba kwa ajili ya nyumba kwa ujumla.

Kisha nikamtaka kuwa dhahiri katika maombi, kuwasilisha hitaji moja baada ya jingine, si kuomba leo kwa kile tutakachokihitaji mwezi ujao au kesho, bali kuomba leo kwa hitaji la leo. Mungu anajibu maombi dhahiri. Mungu hajibu maombi ya jumla.

Usiende kwa Mungu na kusema, “Bwana, okoa jirani zangu.” Badala yake, unaweza kusema, “Baba yangu, namwombea jirani yangu Yohana. Tafadhali gusa moyo wake. Pia, tafadhali nipe hekima na fursa za kujenga urafiki naye na kumfikishia habari njema ya injili.”

Marko 10:47 humwasilisha Batimayo akimwomba Yesu amsaidie. Anaomba, “Yesu Mwana wa Daudi, unirehemu!” Hilo ni ombi la jumla. Katika aya ya 51 Yesu anamtaka kuwa dhahiri: “Wataka nikufanyie nini?” Batimayo akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona.”

Turudi kwenye kisa changu—kijana wetu akaanza kuomba kwa jambo maalum. Alimwomba Mungu amsaidie kupata timu itakayochimba shimo la msingi wa nyumba hiyo. Kisha akaanza kutafuta. Hata hivyo, timu zote alizowasiliana nazo ziliratibiwa miezi kadhaa kabla na zote zilitoza kati ya dola 18,000 na dola 22,000 za kimarekani. Hatimaye alifanikiwa kufanya mazungumzo na timu moja ili kushusha bei hadi kufikia dola 16,000 na kuja juma lililofuata kuchimba msingi.

Kiongozi wa timu hiyo alikuja, lakini mashine kubwa haikuonekana. Baada ya kungoja asubuhi yote, kiongozi huyo alipoteza subira, akasema hangeweza kurudi kwa miezi mitatu na akaondoka. Mwanetu alihuzunika sana. Hakuwa na suluhisho lolote.

Hatimaye, Ovidiu alimwomba Mungu hasa kwa ajili ya timu ya kuchimba shimo haraka na kwa bei nzuri. Alipomaliza sala yake, jirani yake wa karibu alimkaribia.

Jirani: “Habari ya leo.”

Ovidiu: “Salama. Nipo tu natafuta timu ya kuchimba shimo kwa ajili ya msingi wangu.”

Jirani: “Naam, nina timu inayochimba shimo la nyumba yangu hivi sasa. Waulize. Labda wanaweza kufanya na kwako pia.”

Kwa haraka Ovidiu alikimbilia kwa jirani na kuuliza.

Kiongozi wa timu alijibu: “Naam, kwa kuwa tayari tuko hapa na vifaa vyetu vizito, punde tu tunapomaliza hapa, tunaweza kuja kufanya kazi yako.”

Ovidiu: Je! Unaweza kuja kunipa makadirio? Baada ya kuangalia, kiongozi wa timu hiyo alisema, “Nitaifanya kwa dola za kimarekani 2,500.”

Furaha iliyoje! Ovidiu aliona kwamba Mungu alikuwa amekwisha kuandaa jibu na alikuwa akimsubiria Ovidiu kuomba kwa ajili yake. “Maombi ni kuufungua moyo kwa Mungu kama kwa rafiki” (Steps to Christ, uk. 93). Mungu anakuita ili kuwa na mazungumzo ya wazi pamoja Naye, kuwasilisha mahitaji yako kwa njia iliyo wazi na dhahiri kabisa. Anataka uwe na imani Kwake, utarajie majibu kulingana na upendo Wake, hekima na ahadi Yake. Atajibu kwa wakati na kwa njia Yake, lakini ikiwa utamngoja kwa imani, utajua kwamba jibu Lake ni jibu lililo bora zaidi.

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *